Namibia yakosoa kura ya turufu ya Marekani kupinga uanachama wa Palestina katika Umoja wa Mataifa
Namibia imeelezea kusikitishwa kwake kufuatia uamuzi wa hivi majuzi wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa (UNSC) kutopitisha azimio la kuipa Palestina uanachama kamili katika Umoja wa Mataifa.
Katika taarifa, Peya Mushelenga, Waziri wa Mambo ya Nje wa Nambibia, ameelezea kusikitishwa kwake na kura ya turufu iliyotumiwa na Marekani, ambayo ilizuia kupitishwa azimio la kupendekeza uanachama kamili wa Palestina katika Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.
Marekani siku ya Alhamisi ilipiga kura kupinga ombi la Wapalestina la kutaka uanachama kamili wa Umoja wa Mataifa katika kikao cha Baraza la Usalama. Baraza hilo lenye wanachama 15 lilipigia kura rasimu ya azimio lililopendekeza kwa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lenye wanachama 193 kwamba "Nchi ya Palestina ikubaliwe uanachama wa Umoja wa Mataifa."
Rasimu ya azimio hilo ilipata kura 12 za ndio, nchi mbili hazikushiriki na Marekani ilipiga kura ya turufu.
Mushelenga ameikosoa kura hiyo ya turufu kama kurudisha nyuma juhudi za kimataifa zinazolenga kutatua mzozo wa muda mrefu baina ya utawala wa Israel na Palestina.
Mushelenga alisema: "Matumizi ya kura ya turufu katika UNSC kunyima Taifa la Palestina haki yake halali ya uanachama wa Umoja wa Mataifa ni ushuhuda kwamba baadhi ya nchi wanachama wenye nguvu katika Umoja wa Mataifa wanathamini maslahi yao ya kitaifa na hivyo kusababisha uvurugaji wa kanuni za jumuiya ya kimataifa."
Amesisitiza mshikamano wa Namibia na watu wa Palestina na kutoa wito kwa nchi zote za Umoja wa Mataifa zilishinikize Baraza la Usalama la umoja huo ili litekeleze majukumu yake katika kushughulikia suala hilo.