Wataalamu zaidi ya 50 wa UN wataka Israel iwekewe vikwazo na marufuku ya silaha


  • Wataalamu zaidi ya 50 wa UN wataka Israel iwekewe vikwazo na marufuku ya silaha

Wataalamu zaidi ya 50 wa Umoja wa Mataifa wametoa mwito wa kuchukuliwa "hatua madhubuti kimataifa" baada ya kuelezea walivyokasirishwa na shambulio la kinyama la jeshi la utawala wa Kizayuni wa Israel ambalo liliua Wapalestina wasiopungua 45 waliokuwa wametafuta hifadhi kwenye kambi ya muda huko Rafah, kusini mwa Ukanda wa Ghaza.

Wataalamu hao wa UN wamesema: "picha za kutisha za uharibifu, watu kubaki bila makazi na vifo zimeibuka kutoka Rafah, zikiwemo za watoto wachanga walioraruliwa vipandevipande na watu kuteketezwa wakiwa hai".

Kundi hilo la wataalamu zaidi ya 50 wa Umoja wa Mataifa limeendelea kueleza katika taarifa yake kwamba, ripoti zilizotoka kwenye eneo lililolengwa zinaonyesha kuwa shambulio la jeshi la Kizayuni lilikuwa la kiholela na lisilo na mlingano, na lilifanywa wakati watu wakiwa wamekwama ndani wakiungua kwenye mahema ya plastiki, na kusababisha vifo vya kutisha.

Wataalamu hao wa UN wamebainisha kuwa, mashambulizi hayo "ya kinyama" yanaingia kwenye kundi la ukiukaji mkubwa wa sheria za vita, na wakaongeza kuwa wao kwa upande wao wamefadhaishwa sana na jinsi jamii ya kimataifa ilivyoshindwa kukomesha mashambulizi ya Israel dhidi ya Ghaza.

Wataalamu hao wametaka uchunguzi huru ufanyike kuhusu shambulio la Rafah, sambamba na kuchukuliwa hatua za haraka za kuuwekea utawala wa Kizayuni wa Israel vikwazo na marufuku ya silaha.

Aidha wamesema, kueleza kuwa shambulio la Rafah lilifanywa 'kimakosa' hakulifanyi liwe halali wala hakuwarejeshi waliouawa au kuwafariji manusura.

Kundi hilo la wataalamu wa Umoja wa Mataifa limemalizia taarifa yake kwa kusema: "machungu ya watu wa Ghaza lazima yakomeshwe hivi sasa hivi".../

Popular posts from this blog

Jeshi la Wanamaji la Marekani limesema linakabiliwa na vita 'kali zaidi' tangu Vita vya Pili vya Dunia dhidi ya Wayemeni

Hamas yadai kuwakamata wanajeshi wa Israel lakini Israel imekanusha madai hayo