Somalia yapiga hatua kubwa kwa kupata kiti cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa

 .

Somalia imeshinda kiti kisicho cha kudumu katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa - inayosifiwa kama hatua muhimu kwa taifa hilo lililoathirika pakubwa na vita.

Itakuwa ni mara ya kwanza kwa nchi hiyo iliyoingia kwenye vita vya wenyewe kwa wenyewe zaidi ya miaka 30 iliyopita, kushika wadhifa huo tangu miaka ya 1970.

Nafasi hiyo katika Umoja wa Mataifa inaamua jinsi shirika linapaswa kukabiliana na migogoro duniani kote.

Wachambuzi wanasema kuwa jitihada za Somalia kumaliza mgogoro wake na vita vyake dhidi ya wapiganaji wa Kiislamu vitasaidia kufahamisha maamuzi ya Umoja wa Mataifa.

Kuna wanachama 10 wa kupokezana wasio wa kudumu kwenye baraza hilo, pamoja na wanachama watano wa kudumu - Marekani, Uingereza, Ufaransa, China na Urusi.

Ili kushinda kiti, ambacho kina ushawishi mkubwa katika masuala ya ulimwengu, nchi inahitaji kupata uungwaji mkono wa angalau theluthi mbili ya wajumbe wa Baraza Kuu wanaopiga kura.

Somalia ilichaguliwa pamoja na Denmark, Ugiriki, Pakistan na Panama kuhudumu kwa miaka miwili kuanzia Januari mwaka ujao.

Ilishinda kiti hicho kilichotengwa kwa ukanda wa Afrika Mashariki bila kupingwa na kupata kura 179 katika kura ya siri katika Mkutano Mkuu wa wajumbe 193.

Kufuatia kura hiyo, Waziri wa Mambo ya Nje wa Somalia Ahmed Fiqi, ambaye aliongoza ujumbe wa maafisa wa Somalia kwenda New York, alisema nchi yake sasa itachukua "nafasi yake katika jukwaa la kimataifa".

"Tuko tayari kuchukua jukumu muhimu katika kukuza amani na usalama duniani," alisema.

Kuondolewa kwa Mohamed Siad Barre kama rais wa Somalia mwaka 1991 kulizua vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyodumu kwa miongo kadhaa kati ya wababe wa kivita wa koo.

Kwa miaka mingi, Umoja wa Mataifa na Umoja wa Afrika (AU) zimekuwa na majukumu muhimu katika kusaidia kuanzisha tena mamlaka kuu.

Somalia pia imekuwa ikipambana na kundi la wapiganaji wa Kiislamu la al-Shabab, ambalo bado linadhibiti maeneo makubwa ya nchi.

Wapiganaji washirika wa al-Qaeda wanataka kupindua serikali kuu na kuanzisha utawala wao wenyewe kwa kuzingatia tafsiri kali ya sheria za Kiislamu.

Katika miezi ya hivi karibuni, serikali imeongeza mapambano yake dhidi ya kundi hilo huku wanajeshi wa kigeni wakiondoka na kupitisha kijiti hicho kwa jeshi la Somalia.

Popular posts from this blog

Jeshi la Wanamaji la Marekani limesema linakabiliwa na vita 'kali zaidi' tangu Vita vya Pili vya Dunia dhidi ya Wayemeni

Hamas yadai kuwakamata wanajeshi wa Israel lakini Israel imekanusha madai hayo