Waziri Mkuu wa Denmark ashambuliwa mtaani

Mette Frederiksen

Waziri Mkuu wa Denmark Mette Frederiksen anasemekana kushikwa na "mshtuko" baada ya kupigwa na mwanaume mmoja alipokuwa akitembea katikati mwa mji wa Copenhagen.

Shambulio hilo lilifanyika katika eneo la mji mkongwe wa jiji hilo wakati mwanaume huyo alipomkaribia mwanasiasa huyo na kumpiga.

Mtu huyo alikamatwa haraka, lakini hakuna taarifa rasmi kuhusu nia ya kutekeleza kitendo hicho.

Mkuu wa Tume ya Ulaya (EU) Ursula von der Leyen alikitaja kitendo hicho kama “cha kuchukiza, ambacho kinakwenda kinyume na kila kitu tunachoamini na kupigania barani Ulaya".

Tukio hilo linatokea chini ya mwezi mmoja baada ya Waziri Mkuu wa Slovakia Robert Fico kupigwa risasi mara kadhaa alipokuwa akisalimia wafuasi wake. Alinusurika na tangu wakati huo amefanyiwa upasuaji.

Mashahidi wawili, Marie Adrian na Anna Ravn, walielezea shambulio hilo kwenye gazeti la ndani ya taifa hilo la BT, wakisema: "Mwanaume mmoja alitokea upande mwingine na kumsukuma kwa nguvu kwenye bega, na kumfanya aanguke."

Walisema kwamba ingawa " alisukumwa kwa nguvu" waziri mkuu hakujigonga chini wakati wa kuanguka na kwamba aliketi kwenye mgahawa uliokuwa karibu ili kupata nafuu.

Ofisi ya Mette Frederiksen ilisema kuwa tukio hilo limemuacha mwanasiasa huyo akiwa katika "mshtuko".

Polisi wa Copenhagen walisema mwanaume mwenye umri wa miaka 39 atahudhuria kesi katika Mahakama ya Frederiksberg Jumamosi mchana kuhusiana na tukio hilo.

Shambulio hilo linakuja siku mbili kabla ya raia wa Denmark kupiga kura katika uchaguzi wa EU.

Bi Frederiksen, ambaye ni kiongozi wa chama cha Social Democrats cha Denmark, awali alikuwa ameshiriki katika mkutano uliohusu uchaguzi wa Ulaya akiwa na mgombea mkuu wa chama chake Christel Schaldemose.

Popular posts from this blog

Jeshi la Wanamaji la Marekani limesema linakabiliwa na vita 'kali zaidi' tangu Vita vya Pili vya Dunia dhidi ya Wayemeni

Hamas yadai kuwakamata wanajeshi wa Israel lakini Israel imekanusha madai hayo