Khatibu wa Sala ya Ijumaa: Magharibi iwezeshe kufanyika mazungumzo kwa kuheshimu haki za taifa la Iran

 

Nov 29, 2024 12:08 UTC
  • Khatibu wa Sala ya Ijumaa: Magharibi iwezeshe kufanyika mazungumzo kwa kuheshimu haki za taifa la Iran

Khatibu wa Sala ya Ijumaa ya mjini Tehran amesema: "ikiwa Magharibi itarekebisha mwenendo wake na pande mbili zikaheshimiana, itaweza kuandaa mazingira ya kufanyika mazungumzo na kufikia makubaliano na Iran".

Hujjatul-Islam Wal-Muslimin Mohammad Hasan Abu Turabi Fard amesema Iran yenye nguvu daima iko tayari kwa majadiliano na mazungumzo ya kimantiki na ya kielimu, na akaongezea kuwa, ikiwa Magharibi itarekebisha mwenendo wake na pande mbili zikaheshimiana; na ikazingatia haki za taifa adhimu na lenye nguvu la Iran itaweza kuandaa mazingira ya kufanywa mazungumzo na kufikia makubaliano.
 
Khatibu wa Sala ya Ijumaa ya Tehran ameongeza kuwa: Umoja wa Ulaya haunufaiki na sifa ya kuwa taasisi huru na inayojitegemea, kwa sababu maslahi ya Ulaya yamefanywa mhanga wa uchu wa Marekani; na kwa upande mwingine, sera za upendeleo zinazofuatwa katika eneo la Asia Magharibi ni miongoni mwa sababu za kushindikana kujengwa uhusiano thabiti na endelevu na Iran kwa muda wote wa miongo minne sasa.
 
Akiashiria hatua isiyo ya kawaida na ya kiuadui ya Umoja wa Ulaya ya kutoa taarifa ya pamoja na nchi wanachama wa Baraza la Ushirikiano wa Ghuba ya Uajemi na kuzusha madai yasiyo na msingi kuhusiana na visiwa vitatu vya Iran, Hujjatul-Islam Abu Turabi Fard amesisitiza kuwa: nchi za Magharibi zimepata tajiriba ya matukio mawili ya uhalisia katika miongo michache iliyopita; la kwanza ni kwamba, masuala ya eneo la kistratejia la Asia Magharibi hayataweza kutatatuliwa kamwe bila ya kuzingatia maslahi na msimamo wa Iran; na la pili, haiwezekani kuingia katika mazungumzo na Iran yenye nguvu kwa kutumia wenzo wa mashinikizo na vitisho.
 
Khatibu wa Sala ya Ijumaa ya mjini Tehran ameendelea kusisitiza kuwa, nguvu za Muqawama zimewapigisha magoti Wazayuni; na Wazayuni hao hawakuweza kufikia malengo yao yoyote nchini Lebanon; na akaongeza kuwa: Iran ya Kiislamu inajivunia kwamba imekuwa na itaendelea kuwa pamoja na taifa adhimu la Lebanon katika hali zote za shida na raha; na ushindi huo mkubwa kwa mara nyingine tena umedhihirisha kushindwa mashine ya vita ya utawala wa Kizayuni mbele ya macho ya jamii ya kimataifa.../