Russia: Marekani na Uingereza zinaeneza machafuko ndani ya Syria kupitia magenge ya kigaidi

 

Nov 29, 2024 11:41 UTC
  • Russia: Marekani na Uingereza zinaeneza machafuko ndani ya Syria kupitia magenge ya kigaidi

Russia imesema madola makubwa ya Magharibi yanayoongozwa na Marekani yanaendelea na vitendo vyao vya chuki dhidi ya Syria kwa kuwaunga mkono wanamgambo wanaoipinga serikali ya Damascus pamoja na makundi ya kigaidi ya kitakfiri katika kila pembe ya nchi hiyo ya Kiarabu.

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Russia Maria Zakharova amezikosoa Marekani, Uingereza na baadhi ya nchi nyingine za Magharibi kwa kueneza machafuko katika kila pembe ya Syria kupitia makundi ya kigaidi.
 
Zakharova ameongeza kuwa, uungaji mkono wa serikali za Magharibi kwa makundi ya kigaidi yanayoendesha harakati zao katika kila pembe ya Syria si jambo lililobaki kuwa siri bali limeshafichuliwa na liko wazi hadharani.
 
Amesema: "majaribio ya kulilenga taifa la Syria, mamlaka yake ya kujitawala na uhuru wake yamekuwa yakiendelezwa kwa miaka mingi na serikali zinazochukia amani na usalama wa kimataifa kwa ujumla, na zimeichagua Syria na zingali zinaendelea kuing'ang'ania na kuiandama kwa uchokozi na uvamizi wao unaoendelea". 
 
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje wa Russia amebainisha kuwa msimamo wa Moscow wa kuendelea kuiunga mkono Syria na watu wake umekuwa msingi wa kudhamini usalama na utulivu katika eneo la Asia Magharibi.
 
Zakharova ametoa matamshi hayo baada ya ndege za Syria na Russia kushambulia kwa mabomu maficho ya wanamgambo ili kuwarudisha nyuma magaidi wa kitakfiri wanaoungwa mkono na mataifa ya kigeni na wanamgambo wanaoipinga serikali ya Damascus katika eneo la kaskazini magharibi mwa nchi hiyo.
 
Jeshi la Syria limesema linashirikiana na Russia na "vikosi rafiki" kurejesha udhibiti wa maeneo na hali ya mambo kama ilivyokuwa hapo awali.
 
Kwa mujibu wa taarifa ya jeshi hilo, katika msururu wa operesheni za mashambulio walizofanya, askari wa Syria wamewatia hasara kubwa wanamgambo wa kitakfiri wanaoendesha harakati zao katika eneo hilo la kaskazini magharibi mwa nchi.../