Hizbullah ya Lebanon yafanya mashambulio sita dhidi ya ngome na vituo vya kijeshi vya Israel
Muqawama wa Kiislamu wa Lebanon umefanya mashambulio sita dhidi ya ngome na vituo vya kijeshi vya utawala wa Kizayuni wa Israel.
Kabla ya hapo Hizbullah ya Lebanon ilitangaza kupitia taarifa nne tofauti kwamba imefanya shambulio la makombora na mizinga dhidi ya ngome, wanajeshi na zana za kijasusi za utawala wa Kizayuni katika kambi za Bayadh Belida, Roisat Al Alam na Al Raaheb.
Muqawama wa Kiislamu wa Lebanon umelishambulia pia kwa kombora gari la kijeshi la utawala wa Kizayuni katika eneo la al-Mutla na mkusanyiko wa askari wa Kizayuni katika eneo hilo na kuwaangamiza na kuwajeruhi wanajeshi kadhaa.
Kuhusiana na suala hilo, Sheikh Naim Qassem, Naibu Katibu Mkuu wa Hizbullah ameeleza kuwa, harakati hiyo ya Muqawama wa Kiislamu itakabiliana na hatua yoyote ya kushadidisha mivutano itakayochukuliwa na utawala wa Kizayuni na akasisitiza kwa kusema: "hatutaacha kukabiliana na utawala ghasibu wa Israel na kuwaunga mkono wananchi wa Ghaza hadi mapigano yatakaposimamishwa".
Katika kipindi cha miezi michache iliyopita, Hizbullah ya Lebanon imezishambulia ngome za kijeshi za utawala wa Kizayuni kaskazini mwa ardhi zinazokaliwa kwa mabavu zilizopachikwa jina bandia la Israel kufuatia jinai za kinyama na za kutisha na umwagaji mkubwa damu za Wapalestina unaofanya utawala huo katika Ukanda wa Ghaza.
Mashambulio ya Hizbullah yamezusha hofu kubwa kwa Wazayuni wanaoishi katika maeneo hayo.
Hadi sasa makumi ya maelfu ya Wazayuni wamevihama vitongoji vya walowezi karibu na mipaka ya Lebanon kwa kuhofia mashambulizi ya Muqawama.../