Uchina yaishutumu MI6 kwa kuajiri wafanyikazi wa serikali yake
China imelishutumu Shirika la Ujasusi la Uingereza MI6 kwa kuajiri wafanyikazi wa serikali ya China kama majasusi.
Katika chapisho kwenye idhaa yake rasmi ya WeChat, Wizara ya Usalama ya Nchi ya China ilisema watendaji wa MI6 walimgeuza Mchina aliyetambuliwa kwa jina lake la ukoo tu kama Wang na mkewe aliyeitwa Zhou dhidi ya Beijing.
Wote wawili walifanya kazi katika idara za "siri kuu" katika serikali ya Uchina.
Wizara hiyo ilidai kuwa MI6 ilianza kumtumia Bw Wang alipoenda Uingereza kwa masomo yake mwaka wa 2015, chini ya mpango wa kubadilishana wa China na Uingereza.
Wahudumu hao walimchukulia kwa "uangalifu maalum" nchini Uingereza, kama vile kumwalika kwa chakula cha jioni na ziara ili "kuelewa vyema maslahi na udhaifu wake" wizara ilidai.
BBC imeiomba mamlaka ya Uingereza kutoa majibu.
Haya yanajiri muda wa mwezi mmoja tu baada ya Uingereza kuwafungulia mashtaka wanaume wawili kwa kuwa majasusi wa China. Polisi wa Uingereza wamewashutumu kwa kutoa "makala, maelezo, nyaraka au taarifa" kwa taifa la kigeni, huku China ikitaja madai hayo kuwa ni "kashfa mbaya".
Mapema mwezi huu,askari wa zamani wa Wanamaji wa Kifalme aliyeshtakiwa kwa kusaidia huduma ya ujasusi ya Hong Kong alipatikana amekufa, polisi walisema.
Beijing na nchi kadhaa za Magharibi zimezidi kuwa na tuhuma za ujasusi.
Kwa upande wa Bw Wang, mamlaka ya Uchina ilisema wahudumu wa MI6 walichukua fursa ya "tamaa yake kubwa ya pesa" na walifanya urafiki naye chuoni kwa kisingizio kwamba walikuwa wanachuo, na kumfanya atoe "huduma za malipo ya ushauri".